MJAMZITO ADAIWA KUTUPIWA UCHAWI, AZAA MTOTO BUBU.
Stori: Saimeni Mgalula, MBEYA
DUNIA ina
mambo jamani! Mtoto Cecilia Yessa, 6, (pichani) ni bubu na kiziwi tangu
kuzaliwa, lakini baba yake mzazi, Yessa Vincent (39), mkazi wa Kijiji
cha Igawa, Kata ya Lugelele wilayani Mbarali mkoani hapa amesimulia
maajabu yaliyotokea mpaka mtoto wake kupata ulemavu huo.
Akizungumza
na paparazi wetu hivi karibuni nyumbani kwake, baba huyo alisema wakati
mkewe aliyemtaja kwa jina moja la Hafsa akiwa mjamzito, alikumbwa na
mapepo yaliyosababisha kumpiga mwereka mara kwa mara.
AENDA KWA MGANGA WA KIENYEJI
Akiendelea
kuelezea mkasa huo, baba huyo alisema: “Baada ya kuona hali hiyo
ikiendelea kumtokea kwa kasi mke wangu niliamua kwenda kwa mganga wa
kienyeji kuagua ili tujue tatizo ni nini.
“Nilikwenda kwa mganga huyo katika Kijiji cha Muungano ambacho kipo
wilaya hiihii. Mganga aliniambia kuwa, mapepo aliyonayo mke wangu ni ya
mtu ambaye alikuwa ana matatizo ya mikosi ambaye naye alitupiwa dawa
akaogee katikati ya njia panda saa nane usiku huku akiwa ameangalia
upande wa mashariki.
“Mganga aliendelea kuniambia kuwa, mtu huyo aliambiwa dawa hiyo aogee
akiwa mtupu, yaani kama alivyozaliwa huku akisema, ‘nimechoka na kukaa
na mzigo huu naomba nipokelewe na binadamu yeyote au mnyama,’’ alisema
baba huyo akimkariri mganga wake.
MKE APITA, ABEBA UCHAWI
Kwa mujibu wa baba huyo, mganga alimwambia huenda mkewe alipita njia hiyo baada ya mtu huyo kuoga ndipo akapokea mzigo huo.
“Nilipewa
dawa za kumnywesha mke wangu ili kumuepusha na tatizo hilo. Dawa zile
zilimsaidia akaacha kupiga mwereka mara kwa mara na kuonekana ameanza
kupona,” alisema.
MKE AJIFUNGUA, MATATIZO TENA
Yessa
aliendelea kusema kuwa, baada ya miezi tisa mkewe alijifungua mtoto
huyo wa kike. Alizaliwa akiwa vizuri lakini baada ya miezi mitatu mtoto
na mama yake walianza kusumbuliwa tena na matatizo ya mapepo, mama
alikuwa akipiga mwereka kila mara, mtoto naye vivyo hivyo.
“Safari
hii niliamua kuzunguka nao sehemu mbalimbali za waganga wa tiba asilia
ili kuwaepusha na janga hilo, bahati mzuri mganga mmoja alisaidia hali
ikatulia.
CHA AJABU SASA
“Lakini
cha ajabu, baadaye tena tatizo lile likaendelea kumrudia mke wangu.
Mwereka kila wakati. Mbaya zaidi, mtoto wangu naye akaanza dalili za
kutosikia na kushindwa kusema chochote, yaani ni bubu na kiziwi
kwampigo.
“Nachotaka
kusema mpaka nikaamua kutafuta chombo cha habari, hawa waganga
wanautesa sana ulimwengu. Kama kweli mtu anapona, kuondolewa mikosi kwa
kigezo cha watu wengine wabebe mzogo huo ni shida.
“Ni
afadhali basi huo mzigo angebeba mnyama yoyote, hata ng’ombe. Mwanangu
huu ni mwaka wa sita sasa, ni bubu na kiziwi,” alimaliza kusema baba
huyo
0 comments:
Post a Comment