HAYA SASA WAPENZI WA MZIKI WA GOSPEL HHEBU SASA MFAHAMU HUYU

Solomon ambaye pia ni mchungaji anasema kuwa kipaji chake amepewa na Mungu japo anaweka na jitihada zake binafsi. 
Nyimbo zake nyingi anajifunza kutoka kwa waimbaji wa injili Tanzania kwani wana nafasi ya kwanza katika soko la muziki huo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).
Solomon mwenye asili ya DRC akitokea Goma Mashariki mwa mji huo akizaliwa katika familia ya kumjua Mungu japo anasema kuwa baba yake alikuwa na wake wawili. 
Anasema kuwa aliondoka nchini Congo na kuachana na wazazi wake mwaka 2003 ambapo alielekea nchini Uganda na kukaa kwa miaka mitatu na nusu ndipo alipokutana na marehemu Angela Chibalonza aliyemuwezesha na kumpokea Nairobi nchini Kenya. 
“Angela Chibalonza ndiye aliyefungua njia katika maisha yangu ya uimbaji japo wakati nakutana nae nilikuwa katika harakati za kurekodi albamu yangu ya Sijaona rafiki kama Yesu, nimesalia sana katika kanisa la Chibalonza mpaka mauti yanamkuta na siwezi kumsahau ameninyanyua,” anasema. 
Mwimbaji huyo mwenye ndoto nyingi ikiwemo ya kutaka kufungua kituo cha watoto yatima nchini Tanzania anasema kuwa anaipenda sana nchi hii na ndio sababu ya kutoa misaada mara kwa mara. 
“Watanzania hawana mioyo ya kinafiki, ni wakarimu, wacheshi na wenye upendo ndio sababu mimi napenda kuwa Tanzania na kutoa misada ikiwemo kuweka kituo cha kulea watoto yatima” anasema Solomon. 
Solomon Mukubwa anasema akiwa na miaka 12, alipata matatizo ya uvimbe katika mkono wake wa kushoto. 
“Uvimbe huo ulikuwa wa ajabu sana na hakuna aliyefahamu chanzo kilikuwa ni nini? Niliugua kwa muda wa miaka mitatu,”anasema solomon. 
 
Muimbaji huyo anasema wazazi wake walihangaika kumpeleka kwa wataalam wa hospitali mbalimbali na hata kwa waganga wa kienyeji bila mafanikio, na anasema kuwa baada ya muda huo kupita ilianzishwa hospitali moja na Wazungu karibu na nyumbani kwao, na ndipo wataalam wa hapo waliposhindwa na kushauri akatwe mkono kwa lengo la kunusuru uhai wake. 
Solomon anasema ugonjwa wa mkono wake ulitokana na mama yake wa kambo kuwachukia yeye na ndugu zake ndipo mama huyo alitaka kuwaua. 
“Mkono wangu ulivimba sana na baadae ukaoza hiyo ndio sababu ya kukatwa mkono wangu, unajua shetani ni mjinga sana alinitesa kwa miaka mitatu ndiyo sababu ya kuimba wimbo wa Mungu mwenye nguvu,” anasema.
 
 Solomoni aliendelea kusema kuwa hakuna mtu aliyejua kuwa uvimbe huo umetokana na nini lakini hapo baadae ilidhihirika wazi kuwa mama yake wa kambo ndie aliyemroga na kumsababishia tatizo hilo kwani baadae alikuja kukiri na kueleza ukweli. 
Solomoni ambaye kwa sasa maskani yake yapo jiji la Nairobi nchini Kenya anasema wimbo wake wa Mfalme wa Amani aliutunga ili kumtukuza Mungu baada ya kumuepusha na kifo ambacho kingempata baada ya mama yake wa kambo kumroga na kusababisha mkono wake kuvimba na kutibiwa na madaktari bingwa bila mafanikio na hata alipoenda kwa waganga wa kienyeji pia hakupona. 
“Wimbo wangu wa Mfalme wa amani niliamua kuuimba baada kuvuka katika shida hizo na albamu yangu kuipa jina la Mungu mwenye nguvu, na kuna maneno niliweka kwenye kibao hicho kwamba, ukiwa na shida usiende kwa waganga wa dunia, mwite mfalme wa amani, yeye anajibu maombi,” anaeleza Solomoni Mukubwa. 
 
 Baada ya kupona mkono wangu, mama yangu wa kambo alikiri kunifanyia kitendo hicho, lakini mimi nilipookoka nilimsamehe, baada ya muda mfupi naye aliokoka kutokana na pigo kali alilopata kwani mwanaye aliumia jicho alipokuwa anachezea chelewa kwenye moto ambalo uliruka na kuharibu kabisa jicho lake,”anasema. 
Solomoni Mukubwa ambaye ni moja ya waimbaji maarufu wa muziki wa injili Afrika ya Mashariki na Kati alizaliwa miaka 33 iliyopita na ameoa, anasema kuwa anaililia nchi yake na hasa eneo analotoka ndio maana amepanga kwenda kuhubiri ili vita iishe.
“Nawaomba viongozi wa nchi yangu wakae waone ni jinsi gani watasuluhisha na kuwasaidia watu wangu wa Kongo hasa Goma ambako kuna machafuko,”anasema. 
Akizungumzia muziki wa injili kutumika kama biashara anaeleza kuwa huduma ya injili ni kazi kama kazi nyingine lakini cha muhimu ni mtu atawale fedha sio fedha zimtawale. 
Anaeleza pia kuingia studio kunahitaji fedha ila fedha haziwezi kumtenga mtu na Mungu nivema watu wakatambua kuwa muziki wa injili ni ajira tosha kabisa na kusema kuwa kwakwe yeye akipata mahitaji ya muhimu inatosha kabisa kumtumikia Mungu. 
Solomoni ana albamu mbili ambazo ni ‘Sijaona Rafiki, ‘Mungu mwenye nguvu’ na ‘Kwa utukufu wa Mungu.’
 
 

HABARI ZAIDI ZA PADRI ALIYEPIGWA RISASI ZANZIBAR USIKU WA JANA


HABARI ZAIDI ZA PADRI ALIYEPIGWA RISASI ZANZIBAR USIKU WA JANA

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mjini Magharibi Aziz Juma Mohammed amethibitisha kutokea kwa tukio hilo ambalo alisema Father amepigwa risasi na ameumizwa sehemu ya kichwa na amekuwa akitoka damu nyingi kichwani na tayari anapatiwa matibabu katika hospitali kuu ya Mnazi Mmoja.
Alisema jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi wa tukio hilo ili kubaini wahusika walifanya uhalifu huo kwa madhumuni gani kabla ya kuchukuliwa hatua za kisheria.

“Sisi tunahesabu kuwa kitendo hiki ni kitendo cha kihalifu na tunawatafuta wahalifu waliofanya kitendo hiki kwa hivyo bado ni mapema kusema kwamba kitendo hiki kimefanywa na nani kwa kuwa bado uchunguzi wetu unaendelea na hadi sasa hakuna mtu tuliyemshika kuhusikana na tukio hili” alisema Kamanda.



Kamanda Aziz akisimulia tukio hilo alisema walipata taarifa majira ya saa 2 na kwenda katika eneo la tukio ambapo Father alikuwa akitokea kanisani na kutaka kuelekea nyumbani kwake wakati akiwa ndani ya gari ndipo aliposhambuliwa na watu wasiojulikana na kuanguka.

“Tumekuta mabaki ya risasi ndani ya gari yake na katika vioo vyake vya gari vimevunjika na tumekuta damu chini pale” alisema Kamanda.

Aidha Kamanda Azizi alisema Father Ambros yeye ni mhasibu pale kanisani na hivyo mara nyingi watu wananaamini kwamba katika siku za krismass mara nyingi sadaka hukusanywa fedha nyingi na hivyo wanamini kwamba alikuwa fedha mikononi na ndipo inawezekana waliamua kumpiga risasi wakitaka kuchukua fedha hizo.

Hata hivyo alisema uchunguzi wa awali ndio utakaoeleza ni suala gani lililopelekea kupigwa risasi lakini wanaendelea na uchunguzi huo ambapo uchunguzi ndio utakaojulikana sababu kamili ya tukio hilo.

Akizungumzia tukio hilo, Askofu Michael Hafidh wa Kanisa la Anglikan la Mkunazini amesema wamesikitishwa na wamepokea kwa mshituko mkubwa tukio hilo hasa kwa kuzingatia matukio kama hayo hayajawahi kutokea ya kuwahujumu viongozi wa dini.


Alisema tukio hilo ni miongoni mwa matukio ya kushtusha na yanaashiria hali mbaya ya kiusalama na kuwaomba viongozi wa serikali kuchukua hatua za tahadhari kubwa kwani matukio kama hayo yameanza kutokea kwa viongozi wa dini ambapo mwanzo ilianzia kwa Sheikh Soraga na baadae kutokea kwa Father Ambros.

“ Hii ni hali ya hatari katika nchi yetu na haipendezi lakini serikali lazima ijue sisi hatuwezi kujua wala hatuwezi kujilinda lakini serikali inapaswa kutulinda sisi ndio wananchi wake” alisema Askofu Hafidh.

NURU FM 93.5 IRINGA

.

.

.

Nyali

Pages

Pages

Powered by Blogger.

Search This Blog