Wizara
ya Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki Kikanda na Kimataifa
imejipanga kuwapeleka kwenye Balozi zake nje Watumishi wapatao 105 na
kuwarejesha nchini wengine 79 ambao miongoni mwao muda wao wa utumishi
balozini (Tour of Duty) umemalizika na wengine kustaafu kwa mujibu wa
sheria za Utumishi wa Umma. Kwa kawaida tour of duty kwa Watumishi nje
ni ya muda wa miaka minne (4).
Tanzania
ina Balozi 35 nje ya nchi ambazo kwa ujumla wake zina Watumishi 234.
Miongoni mwa Watumishi watakaorejea nchini wamo Mabalozi, Maafisa,
Wahasibu na Makatibu Muhtasi.
Hadi
sasa Mabalozi waliorejea nchini ni watatu (3) ambao ni Balozi Peter
Kalaghe aliyekuwa Uingereza, Balozi James Msekela aliyekuwa Italia na
Balozi Batilda Burian aliyekuwa Japan.
Itakumbukwa
kuwa, Januari 25, 2016 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.
Dkt. John Pombe Magufuli aliiagiza Wizara ya Mambo ya Nje, Ushirikiano
wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa kuwarejesha nyumbani mara moja
Mabalozi hao ambao mikataba yao iliisha na wengine kwa ajili ya
kupangiwa majukumu mengine.
Aidha,
jumla ya Watumishi tisa wa kada mbalimbali waliokuwa Balozini
wamerejea nchini hadi sasa na wengine wanaendelea kurejea kulingana na
upatikanaji wa fedha kwa ajili ya kufanikisha jukumu hilo.
Utaratibu
wa kuwapeleka na kuwarejesha Watumishi Balozini ni wa kawaida na upo
duniani kote kwa mujibu wa sheria za kimataifa ukiwemo Mkataba wa Vienna
unaotoa mwongozo kwenye masuala ya kidiplomasia.
Wizara itaendelea kupeleka Watumishi wenye sifa na tija kwa taifa ili kuiwakilisha nchi kikamilifu.
WAKATI HUOHUO,
Waziri wa Viwanda na Biashara wa Oman Mhe. Dkt. Ali Bin Masoud Al
Sunaidy alifanya ziara ya kikazi nchini Tanzania kuanzia tarehe 12
April hadi 14 April, 2016.
Lengo
la ziara hiyo lilikuwa ni kushiriki Kongamano la Biashara na Uwekezaji
baina ya Tanzania na Oman, kongamano hili lilikuwa na kauli mbiu ya ‘’
Oman Tanzania Road show : Exploring Opportunities in Investment and
Business between Tanzania and Oman’’.
Ziara
na kongamano hili imelenga zaidi katika sekta za Madini, Kilimo na
uboreshaji wa mazao ya Kilimo, Mifugo, Miundombinu na Mawasilisno,
Uvuvi, Usafirishaji, Utalii, Petroli na Gesi. Mgeni Rasmi katika
kongamano hili alikuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Mhe. Samia Suluhu Hassan
Katika
ziara hii, Mhe. Waziri Al Sunaidy aliongozana na ujumbe wa watu 108
ambapo 12 walikuwa ni Maafisa kutoka Taasisi mbalimbali za Serikali ya
Oman na wengine waliobaki kutoka Sekta Binafsi kutoka nchi hiyo kwa
lengo la kukutana na Taasisi kama hizo hapa nchini.
Kwa
upande wa Tanzania wafanyabiashara 190 walishiriki na wenzao kutoka
Oman katika kongamano na baadae katika mikutano ya ana kwa ana (Business
to Business meetings).
0 comments:
Post a Comment