Home » » Trilioni 1 Yatengwa Ili Kuyaondoa Malori ya Mizigo Dar

Trilioni 1 Yatengwa Ili Kuyaondoa Malori ya Mizigo Dar


Malori  ya kubeba mizigo, ambayo yamekuwa yakichangia msongamano wa magari kwa kiasi kikubwa jijini Dar es Salaam, yanatarajiwa kuondolewa mara tu reli ya kisasa ‘Standard Gauge’, iliyotengewa Sh trilioni moja katika Bajeti ya Serikali, itakapofika Ruvu mkoani Pwani.

Rais John Magufuli amesema hayo jana wakati akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa barabara ya kwanza ya juu (Flyover) nchini Tanzania, inayojengwa katika makutano ya Barabara ya Mandela na Barabara ya Nyerere eneo la Tazara, kwa ufadhili wa Serikali ya Japan.

Barabara hiyo ya juu kwa mujibu wa taarifa za Wakala wa Barabara (Tanroads), ikikamilika inatarajiwa kupunguza muda wa magari kukatiza katika makutano hayo kwa asilimia 80, kutoka wastani wa dakika 45 hadi dakika 10 tu kwa wanaotoka upande mmoja kwenda mwingine.

Akifafanua zaidi kuhusu reli, Rais Magufuli alisema fedha hizo zimetengwa katika bajeti itakayopelekwa katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, linalotarajiwa kuanza vikao vyake wiki ijayo, ili ujenzi uanze kwa fedha za ndani wakati wafadhili wa kusaidia kuendeleza wakitafutwa na wakipatikana, wakute reli hiyo imeanza kujengwa.

Kwa mujibu wa Rais Magufuli, reli hiyo itakapofika Ruvu, kutajengwa bandari kavu kubwa ambayo ikikamilika, mizigo yote inayoshuka Bandari ya Dar es Salaam, itasafirishwa kwa reli mpaka katika bandari hiyo na malori yanayochukua na kupeleka mizigo katika bandari hiyo, yataishia katika bandari hiyo kavu.

Ili kuepuka wizi wa mizigo, Rais Magufuli alisema kutafungwa kamera katika njia yote ya reli mpaka Ruvu, ili kontena linaloshushwa katika Bandari ya Dar es Salaam, lifuatiliwe mpaka katika bandari hiyo.

Mbali na reli hiyo ambayo ikikamilika kwa mujibu wa taarifa za Mamlaka ya Bandari (TPA), itapunguza gharama za usafirishaji wa mizigo kwa asilimia 30 na kuongeza kivutio cha bandari hiyo duniani, Rais Magufuli alisema Mfuko wa Barabara utatoa fedha za kujenga barabara za pete, zitakazoongeza kasi ya kupunguza msongamano kama si kuumaliza.

Alionya kuwa fedha za Mfuko wa Barabara si za kulipana posho, bali kutengeneza barabara hizo za pete katika halmashauri na kuagiza makandarasi wanaotoa asilimia 10 kwa ajili ya rushwa, wasipewe zabuni bali watafute makandarasi wazuri.

Alisema kilometa 27 za barabara hizo za pete, zimeanza kujengwa na kwa kuwa wabunge wa Dar es Salaam waliopita walisema sana, waliongezewa kilometa nyingine 86 za barabara hizo za pete, zitakazojengwa kwa lami kwa fedha za mfuko huo.

Malori kutaifishwa 
Pia Rais Magufuli ameagiza halmashauri za Dar es Salaam kuweka sheria itakayokataza kupitisha magari yenye tani zaidi ya 56 katika barabara hizo, yakiwemo malori ili barabara hizo zilizokusudiwa kutumika na magari madogo, zisiharibiwe na magari yenye uzito mkubwa.

“Hakuna kupitisha magari yenye tani zaidi ya 56 na mtu akipitisha kamateni gari na ikiwezekana litaifishwe kabisa ili ajifunze kutopita katika barabara hizo na kuziharibu,“ alisisitiza.

Akizungumzia miradi hiyo ya kupunguza msongamano ikiwemo barabara za juu ikiwemo ya Ubungo, Rais Magufuli alisema zitapunguza hasara iliyokuwa ikitokea kwani katika utafiti wa mwaka 2013, ulionesha kuwa Jiji la Dar es Salaam pekee lilipoteza Sh bilioni 411.3 katika msongamano wa magari.

Mbali na hasara hiyo iliyooneshwa katika utafiti, Rais Magufuli alisema inawezekana kabisa msongamano wa magari Dar es Salaam umesababisha baadhi ya watu kufa kwa kuchelewa kufikishwa hospitalini na baadhi ya ndoa kuvunjika kutokana na kuchelewa kufika nyumbani na kushindwa kujieleza.

Rais alisema msongamano ni tatizo na kama siyo kumaliza basi lazima lipunguzwe kabisa kwa kuwa Dar es Salama ndiyo kioo cha Tanzania, ambapo mizigo inayotoka na kwenda nchi zisizo na bandari inapita hapo.
Facebook Blogger Plugin: Bloggerized by Joseph Kipangula Enhanced by Joseph Kipangula

0 comments:

Post a Comment

NURU FM 93.5 IRINGA

.

.

.

Nyali

Pages

Pages

Powered by Blogger.

Blog Archive

Search This Blog