Kamati
maalumu ya uchunguzi iliyoundwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul
Makonda imefichua madudu na harufu ya ufisadi katika utekelezwaji wa
mikataba mitatu, inayohusu maeneo ya ukusanyaji mapato ya Stendi Kuu ya
Mabasi Yaendayo Mikoani ya Ubungo na kodi ya uegeshaji magari katikati
ya mji.
Kutokana
na madudu hayo, Mkuu huyo wa Mkoa amebainisha wazi kuwa hataki kufanya
kazi tena na Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, Wilson Kabwe na Kaimu
wake, Sarah Yohana na kuwasilisha majina yao kwa mamlaka husika ya
nidhamu kwa hatua zaidi.
Akizungumza
na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, alisema hivi karibuni
aliunda kamati hiyo maalumu kufuatilia maeneo hayo muhimu kutokana na
malalamiko ya muda mrefu, ambayo ofisi yake ilikuwa ikipokea kutoka kwa
wananchi.
Alisema
kwa mujibu wa uchunguzi, kamati hiyo ilibaini kuwa katika stendi ya
mabasi ya Ubungo, kumekuwa na ubadhirifu mkubwa wa fedha za umma,
ikiwemo kutokuwasilishwa kwa mapato halisi yanayotokana na makusanyo ya
kila siku serikalini.
“Kamati
ile imebaini kuwa pale ubungo kunatumika sheria ndogo mbili za
ukusanyaji mapato moja ya mwaka 2004 na nyingine mwaka 2009 kwa lengo la
kunufaisha wachache,” alisema Makonda.
Alifafanua
kuwa Sheria Ndogo ya Mwaka 2004 ya ukusanyaji mapato ndani ya kituo
hicho, inaonesha kuwa kila basi linatakiwa kutozwa Sh 4,000, hivyo
makusanyo halisi kwa mwezi ni Sh milioni 42 kutokana na mabasi 350
yanayoegeshwa kituoni hapo.
Hata
hivyo, alisema kutokana na mabadiliko ya tozo, sheria hiyo
ilibadilishwa mwaka 2009 na kila basi likawa linatozwa Sh 8,000 na hivyo
makusanyo ya mwezi yakapanda na kufikia Sh milioni 82 kwa mwezi.
“Lakini
cha kushangaza tumebaini kuwa bado kampuni inayokusanya mapato katika
kituo cha Ubungo, inawasilisha mapato hayo kwa kutumia sheria ya mwaka
2004 yaani Sh milioni 42 badala ya Sh milioni 82 kwa mwezi…”
“…Mbaya
zaidi kamati ile katika ukaguzi wake, ilikuta kampuni ya ukusanyaji
mapato hayo stendi ya Ubungo inayo Sheria ya Mwaka 2009 lakini katika
nyaraka za Halmashauri ya Jiji zinaonesha sheria inayotumika ni ya mwaka
2004,” alisisitiza Makonda.
Alisema
katika uchunguzi ilibainika kuwa kampuni iliyo chini ya Halmashauri ya
Jiji inayokusanya mapato hayo stendi ya Ubungo, ilisaini mkataba wa
ukusanyaji mapato hayo kwa mara ya kwanza Januari 31, 2004 na baadaye
ikasaini tena mkataba Januari 30, mwaka jana.
Kwa
mujibu wa Makonda, kwa hali ilivyo tangu Sheria Ndogo ya Mwaka 2009
ipitishwe, haijawahi kutumika na hivyo kulisababishia hasara jiji hilo
ya Sh bilioni tatu kutokana na mapato katika stendi hiyo kuendelea
kuwasilishwa kwa kutumia sheria ya mwaka 2004.
“Ukipiga
hesabu za harakaharaka utagundua kuwa kila mwezi Sh milioni 42 zimekuwa
zikipotelea kwenye mikono ya wachache, kwa maana hiyo kuanzia mwaka
2009 Sh bilioni tatu zimepotea na kila mwaka tumekuwa tukipoteza Sh
milioni 500, huu ni ufisadi wa aina yake kwa kweli,” alisema.
0 comments:
Post a Comment