Home » » Vigogo Jiji la Dar es Salaam Wakalia Kuti Kavu....Makonda Afichua Siri Mikataba Tata, Ataka Mamlaka za Uteuzi Ziwaondoe

Vigogo Jiji la Dar es Salaam Wakalia Kuti Kavu....Makonda Afichua Siri Mikataba Tata, Ataka Mamlaka za Uteuzi Ziwaondoe

 
Kamati maalumu ya uchunguzi iliyoundwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda imefichua madudu na harufu ya ufisadi katika utekelezwaji wa mikataba mitatu, inayohusu maeneo ya ukusanyaji mapato ya Stendi Kuu ya Mabasi Yaendayo Mikoani ya Ubungo na kodi ya uegeshaji magari katikati ya mji.

Kutokana na madudu hayo, Mkuu huyo wa Mkoa amebainisha wazi kuwa hataki kufanya kazi tena na Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, Wilson Kabwe na Kaimu wake, Sarah Yohana na kuwasilisha majina yao kwa mamlaka husika ya nidhamu kwa hatua zaidi.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, alisema hivi karibuni aliunda kamati hiyo maalumu kufuatilia maeneo hayo muhimu kutokana na malalamiko ya muda mrefu, ambayo ofisi yake ilikuwa ikipokea kutoka kwa wananchi.

Alisema kwa mujibu wa uchunguzi, kamati hiyo ilibaini kuwa katika stendi ya mabasi ya Ubungo, kumekuwa na ubadhirifu mkubwa wa fedha za umma, ikiwemo kutokuwasilishwa kwa mapato halisi yanayotokana na makusanyo ya kila siku serikalini.

“Kamati ile imebaini kuwa pale ubungo kunatumika sheria ndogo mbili za ukusanyaji mapato moja ya mwaka 2004 na nyingine mwaka 2009 kwa lengo la kunufaisha wachache,” alisema Makonda.

Alifafanua kuwa Sheria Ndogo ya Mwaka 2004 ya ukusanyaji mapato ndani ya kituo hicho, inaonesha kuwa kila basi linatakiwa kutozwa Sh 4,000, hivyo makusanyo halisi kwa mwezi ni Sh milioni 42 kutokana na mabasi 350 yanayoegeshwa kituoni hapo.

Hata hivyo, alisema kutokana na mabadiliko ya tozo, sheria hiyo ilibadilishwa mwaka 2009 na kila basi likawa linatozwa Sh 8,000 na hivyo makusanyo ya mwezi yakapanda na kufikia Sh milioni 82 kwa mwezi.

“Lakini cha kushangaza tumebaini kuwa bado kampuni inayokusanya mapato katika kituo cha Ubungo, inawasilisha mapato hayo kwa kutumia sheria ya mwaka 2004 yaani Sh milioni 42 badala ya Sh milioni 82 kwa mwezi…” 
“…Mbaya zaidi kamati ile katika ukaguzi wake, ilikuta kampuni ya ukusanyaji mapato hayo stendi ya Ubungo inayo Sheria ya Mwaka 2009 lakini katika nyaraka za Halmashauri ya Jiji zinaonesha sheria inayotumika ni ya mwaka 2004,” alisisitiza Makonda.

Alisema katika uchunguzi ilibainika kuwa kampuni iliyo chini ya Halmashauri ya Jiji inayokusanya mapato hayo stendi ya Ubungo, ilisaini mkataba wa ukusanyaji mapato hayo kwa mara ya kwanza Januari 31, 2004 na baadaye ikasaini tena mkataba Januari 30, mwaka jana.

Kwa mujibu wa Makonda, kwa hali ilivyo tangu Sheria Ndogo ya Mwaka 2009 ipitishwe, haijawahi kutumika na hivyo kulisababishia hasara jiji hilo ya Sh bilioni tatu kutokana na mapato katika stendi hiyo kuendelea kuwasilishwa kwa kutumia sheria ya mwaka 2004.

“Ukipiga hesabu za harakaharaka utagundua kuwa kila mwezi Sh milioni 42 zimekuwa zikipotelea kwenye mikono ya wachache, kwa maana hiyo kuanzia mwaka 2009 Sh bilioni tatu zimepotea na kila mwaka tumekuwa tukipoteza Sh milioni 500, huu ni ufisadi wa aina yake kwa kweli,” alisema.
Facebook Blogger Plugin: Bloggerized by Joseph Kipangula Enhanced by Joseph Kipangula

0 comments:

Post a Comment

NURU FM 93.5 IRINGA

.

.

.

Nyali

Pages

Pages

Powered by Blogger.

Blog Archive

Search This Blog